Header Ads

Breaking News
recent

VIPODOZI HATARI VYATEKETEZWA TANI NZIMA NA TFDA.



MAMLAKA ya Chakula na Dawa (TFDA) katika Kanda ya Ziwa, imekamata vipodozi vyenye viambato vinavyoathiri afya za watumiaji katika Wilaya ya Bunda, mkoani Mara.

Vipodozi hivyo vina  thamani ya zaidi ya Sh10 milioni na tayari vimeteketezwa kwa moto.
Mkaguzi wa Dawa katika mamlaka hiyo Kanda ya Ziwa, Mtani Njegere, alisema vipodozi hivyo vilikamatwa juzi katika maduka mbalimbali ya mjini Bunda.
Njegere alisema vipodozi hivyo vilikuwa na uzito wa zaidi ya tani moja na thamani yake ni zaidi ya Sh10 milioni.

Alisema vipodozi hivyo vimeteketezwa chini ya vyombo vya ulinzi na usalama wilayani humo. Aliongeza kuwa TFDA katika kipindi cha  wiki tatu mfululizo, imefanya zoezi hilo mkoani humo.
“Kwa muda wa wiki tatu tumeendesha zoezi hili katika wilaya zote za Mkoa wa Mara, tumefanikiwa kukamata vipodozi vilivyopigwa marufuku na Serikali,” alisema.

Alisema katika wilaya nyingine hawakufanikiwa kuvikamata vipodozi hivyo kutokana na wafanyabiashara kuvificha.

Alisema kuwa wafanyabiashara waliokamatwa na vipodozi hivyo walionywa baada ya kujitetea kwamba walivinunua bila ya kujua.

Mkaguzi huyo alitoa wito kwa wananchi hususan wanawake, kuwa makini  wanaponunua vipodozi madukani, kwa sababu vingi ni feki na tayari vimepigwa marufuku.

Alisema kutokana na hali hiyo, TFDA imeweka dira ya miaka mitano kwa ajili ya kukabiliana na tatizo hilo.

Ofisa Mazingira wa Halmashauri ya Wilaya ya Bunda, Nashoni Stafa, na Ofisa mifugo katika halmashauri hiyo, Rick Kaduri, walisema zoezi hilo linapaswa kuwa endelevu kwa kuzingatia kuwa bidhaa feki zimezagaa kila kona.

No comments:

KARIBU UTOE MAONI YAKO HAPA

Powered by Blogger.