Header Ads

Breaking News
recent

UGAWAJI ARDHI KWA WAGENI KIHOLELA UTALIANGAMIZA TAIFA.


Halima Mdee - Mbunge
MBUNGE wa Kawe, Halima Mdee jana aliwasilisha hoja binafsi bungeni, akitaka Serikali isitishe ugawaji wa ardhi kwa wageni hadi hapo itakapokuwa imefanya tathmini na kujiridhisha kwamba wananchi watakuwa na ardhi ya kutosha kwa kilimo cha mazao ya chakula na matumizi mengine ya kuendeleza shughuli za maendeleo.

Mbunge huyo ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, pamoja na kuituhumu Serikali kwa kuwakumbatia wawekezaji ambao alisema wanapora ardhi ya wananchi, alisema ugawaji huo holela wa ardhi kwa wageni usipositishwa haraka ardhi yote nzuri itachukuliwa na wageni.

Tunampongeza mbunge huyo kwa kupeleka hoja hiyo muhimu bungeni, hasa tukiangalia umuhimu wa suala la ardhi siyo tu katika muktadha wa amani na utulivu katika nchi yetu, bali pia katika ustawi na maendeleo ya wananchi ambao asilimia kubwa inategemea ardhi kwa ajili ya kilimo. Lakini pia tunawapongeza wabunge wote waliochangia hoja hiyo kwa kuzingatia maslahi ya taifa bila kuendekeza mitazamo ya kisiasa na kiitikadi.

Ni bahati mbaya kwamba suala la ardhi limekuwa likitazamwa  kisiasa tangu Serikali ya Awamu ya Kwanza ilipoondoka madarakani. Kama ilivyokuwa kwa Azimio la Arusha ambalo lilipigwa teke mara baada ya awamu hiyo kukabidhi Serikali kwa awamu nyingine, viongozi waliokabidhiwa madaraka walifuta misingi muhimu iliyokuwa ikisimamia suala la ardhi ambalo Azimio la Arusha lilikuwa limelipa umuhimu wa pekee kwa lengo la kulinda umoja na amani ya nchi yetu.

Waasisi wa Azimio hilo waliangalia mbele na kugundua kwamba suala la ardhi ni suala la kufa na kupona. Nchi yetu haiwezi kuwa na amani ya kudumu kama wananchi wake watakosa ardhi ya kuwawezesha kuendesha maisha yao kwa njia ya kilimo au ufugaji. Hii ni kwa sababu kilimo ndiyo uti wa mgongo wa asilimia zaidi ya 80 ya wananchi ambao wanaishi vijijini.

Hivyo tunakubaliana kabisa na mtoa hoja kwamba kuna umuhimu mkubwa wa kufanya tathmini ili kubaini raia wa kigeni na wa ndani waliochukua ardhi kinyemela. Siyo siri kwamba ukwapuaji huo wa ardhi umefanyika kutokana na viongozi wengi wa Serikali za Vijiji kupokea rushwa kutoka kwa wageni hao, kinyume cha Sheria ya Ardhi Namba 5 ya mwaka 1999.

Miaka ya hivi karibuni tumeshuhudia utitiri wa watu hao wakiwarubuni viongozi hao wa vijiji na kufanikiwa kutwaa sehemu kubwa za ardhi kwa bei ya kutupwa, huku wakiwaacha wananchi hao katika umaskini wa kutisha. Nani asiyejua kwamba wengi wa watu hao wanaojiita wawekezaji wameshindwa kuendeleza ardhi waliyoitwaa hadi leo? Pia nani asiyejua kwamba baadhi yao, pamoja na kuchukua ardhi kubwa kwa bei ndogo, waliuza ardhi hiyo kinyemela kwa bei ya kutisha hata bila kulipa kodi ya Serikali?

Tunakubaliana na mtoa hoja kwamba tatizo hilo kwa kiasi kikubwa limesababishwa na Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi kutokana na kutokudhibiti hali hiyo kwa kufanya tathmini ili kupata takwimu kwa lengo la kujua ukubwa wa tatizo. Kutofanya hivyo kumesababisha migogoro ya ardhi isiyokwisha katika kila pembe ya nchi yetu na kuwaacha baadhi ya wananchi wakiwa kama wakimbizi katika nchi yao.

Kama tulivyosema hapo juu, Serikali nayo imekuwa sehemu ya tatizo kwa kuchukua ardhi ya wananchi na kuwapa wawekezaji pasipo kwanza kulipa fidia. Wilaya zilizoathirika ni nyingi.

Moja ya wilaya ambazo wananchi wake wameathirika ni Bagamoyo, ambapo Serikali ilitwaa kwa nguvu ardhi ya wakazi wa Kijiji cha Zinga miaka minne iliyopita kwa kisingizio cha kutenga eneo la wawekezaji cha EPZ na mpaka leo imeshindwa kuwalipa fidia.

Hapo ndipo mahali pa kuanzia. Haiwezekani Serikali ile njama na wawekezaji kupora ardhi ya wananchi pasipo kuwalipa fidia kwa kisingizio cha kukaribisha wawekezaji. Hali hiyo itakaribisha ghasia na vurugu.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:

KARIBU UTOE MAONI YAKO HAPA

Powered by Blogger.