Header Ads

Breaking News
recent

AJALI MBEYA YAUWA WATU SITA HAPO HAPO.

BASI AINA YA TOYOTA HIACY  YENYE NAMBA ZA USAJIRI T245 AMH ILIYOGANWGA NA ROLI LA MIZIGO


JINAMIZI la ajali mkoani Mbeya limeendelea kumaliza roho za watu baada ya watu  sita kupoteza maisha  na wengine 10 kujeruhiwa katika ajali iliyotokea eneo la Itewe, Kata ya Inyala, Wilaya ya Mbeya Vijijini.


HILI NDILO ROLI LILILOSABABISHA AJALI NA KUUA ABIRIA SITA


Tukio hilo lilitokea jana saa 4:00 asubuhi katika  ajali iliyohusisha basi dogo la abiria  aina ya Toyota Hiace lililokuwa likitokea mjini Mbeya kwenda Chimala wilayani Mbarali na lori  aina ya FAW   lenye  tela  lililokuwa likitokea Dar es Salaam kwenda nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.

Katika ajali hiyo, watu watano walifariki papohapo na mmoja alifariki akiwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mbeya alikopelekwa kupatiwa huduma.


BAADHI YA MAJERUHI WAKIFIKISHWA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA MBEYA.
Akithibitisha  kupokea miili ya marehemu na majeruhi hao, Ofisa  Muuguzi wa  Kitengo cha Huduma za Dharura, Jenny Kapeye alisema kuwa alipokea miili ya marehemu watano waliofariki eneo la tukio na mmoja alifariki akiwa anapatiwa huduma hospitalini hapo.
                           
Aliwataja waliopoteza maisha katika ajali hiyo kuwa ni Steven Kimario,  Shalfa Abdallah, Simon Mwakalikwa, Andrew Simbeye, Mariam Mwanginde  na mwanamume mwingine ambaye hakufahamika jina lake mara moja.

Miili yote imehifadhiwa katika hospitali hiyo ya rufaa.

Majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo ni 10 na kati yao saba walitibiwa na kuruhusiwa huku watatu ambao ni Elia Malowe, Charles Gumani na Doto Tagala wamelazwa wodini.

Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya, Diwani Athumani alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo ambapo alisema kuwa uchunguzi wa awali ulibaini kwamba  dereva wa lori hilo alikuwa akiendesha gari huku akiwa amelewa pombe  aina ya Konyagi.

Kwa mujibu wa Kamanda Athumani, pombe hiyo ilikutwa ndani ya gari hilo na wananchi waliofika kutoa msaada na baada ya kugundua hilo ulizuka mgogoro mkubwa uliosababisha dereva huyo kutaka kupigana na wananchi hao.

Kamanda Athumani alisema Jeshi la Polisi linamshikilia dereva huyo kwa uchunguzi zaidi.

Ajali hiyo imekuja ikiwa ni siku 40 tangu kutokea ajali nyingine mkoani humo iliyosababisha watu 10 kufariki dunia na wengine 25 kujeruhiwa akiwamo Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Mery Mwanjelwa baada ya lori la mafuta kushindwa kufunga  breki na kuyagonga magari mengine matatu katika mteremko wa Mlima wa Iwambi – Mbalizi nje kidogo ya Jiji la Mbeya.

Picha na LUKAZA BLOG.

No comments:

KARIBU UTOE MAONI YAKO HAPA

Powered by Blogger.