Header Ads

Breaking News
recent

MKUTANO WA MAPINDUZI YA KIJANI AFRIKA (AGRA) KUFANYIKA ARUSHA MWEZI HUU.

Asili Yetu © All rights reserved

Rais wa AGRA Bi. Jane Kaluku (katikati) akifuatiwa na Mkurugenzi wa mfuko wa AGRA Bi. Anne Mbaabu (kushoto) na mwisho ni muwakirishi wa AGRA nchini Bwana.Fredy Muhhuku wakiwa wanazungumza na waandishi wa habari kuhusu mkutano huo utakao anza mwezi huu.


Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa jukwaa la mapinduzi ya kijani Afrika utakaofanyika kuanzia  Septemba 26 hadi Septemba 28 mjini Arusha. Mkutano huo utawakutanisha viongozi mbali mbali wa kimataifa ambao watajadili namna ya kuchukua hatua katika kuboresha usalama wa chakula duniani.


Aidha katika mkutano huo viongozi hao wataweza kujadili  sera ya mapinduzi ya kilimo na uchumi wa Afrika ,njia za kukuza masoko pamoja na namna ya kubadilisha mfumo wa kilimo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa Rais wa umoja wa mapinduzi ya kijani Afrika (AGRA) bi Jane  Karuku  alisema kuwa mkutano huo ni hatua inayofuata katika kuendeleza bara  la Afrika kupata ufumbuzi katika masuala ya usalama wa chakula.

Karuku alisema kuwa Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huo katika kukuza sekta ya ukuaji wa kilimo inawakilisha uchunguzi  uliofanywa katika wilaya ya kilombero mkoa wa morogoro juu ya njia bora za kilimo.
Alieleza kuwa uchunguzi huo uliwezesha uzalishaji wa mahindi kwa wakulima wadogo wa wilaya hiyo kuongezeka kutoka tani 1.5 hadi 4.5 kwa hekta ,ambapo kwa upande wa mavuno ya mpunga yaliongezeka kutoka tani 2.5 hadi tani 6  hali iliyopelekea Tanzania kupata fursa hii  ya kuwa mwenyeji wa mkutano huo.

Aidha alisema kuwa jukwaa hilo litatoa nafasi ya kujadili namna bora ya kuendeleza mipango ya uwekezaji wenye tija kwa ajili ya kuongeza  maendeleo ya kilimo barani Afrika pamoja na kujadili namna bora ya kuunganisha nguvu ya jamii na sekta binafsi katika kuboresha usalama wa chakula duniani

Aliongeza kuwa jukwaa hilo pia litaweza kujadili na kutafuta njia bora za kuboresha kilimo barani Afrika na kuwawezesha wakulima wadogo wadogo  kushirikiana na vyama vya ushirika na wadau wengine ambapo mjadala huo utatoa njia bora za matumizi ya rasilimali na kukabiliana na changamoto zinazowakabili  mamilioni ya wakulima barani Afrika.

“Wakulima wadogo wadogo ni kitovu kwa yale yote tuyafanyayo hivyo mtazamo wetu ni kuwapatia wakulima wa afrika dhana za kilimo wanazohitaji ili waweze kukua zaidi na kuongeza kipato chao na watatuongoza katika kupata mafanikio mazuri”Alisema bi Jane



No comments:

KARIBU UTOE MAONI YAKO HAPA

Powered by Blogger.