RAIS KIKWETE AKEMEA VITENDO VYA WANAOENEZA UDINI KATIKA JAMII.
Rais Jakaya Kikwete amewaonya baadhi ya wananchi wakiwemo wanasiasa
na viongozi wa dini wanaoeneza udini katika jamii na siasa kuwa jambo
hilo ni hatari kwa usalama wa nchi na amewataka waache mara moja kwani
vinginevyo watawagawa watanzania na kuiingiza nchi katika machafuko na
mauaji kwa agenda isiyokuwa ya watanzania.
Akiongea na viongozi wa ngazi mbalimbali za wilaya na mkoa wa
Kagera na wananchi kwenye mkutano wa majumuisho ya ziara yake mkoani
Kagera rais Kikwete amesema agenda ya udini inayoenezwa na watu
mbalimbali siyo agenda ya Watanzania bali inaletwa na watu wenye nia
mbaya wanaoionea wivu Tanzania kutokana na amani na utulivu ulioko
nchini.
Rais Kikwete ametumia fursa hiyo kuwaomba viongozi wa dini
madhehebu yote wakristo na waislamu kuendelea kuwahubiria Watanzania
kuhusu umuhimu wa amani, umoja na mshikamano na amesema ikiwa dini
itaingizwa kwenye siasa, itafika wakati nchi itagawanywa kwa udini
ambapo hata viongozi watachaguliwa kwa misingi ya dini jambo ambalo ni
hatari na litaleta misukosuko na mifarakano katika jamii.
Aidha rais Kikwete amezungumza kwa uzito mkubwa kuhusu wahamiaji
haramu ambao amesema lazima waondoke nchini kwani walipewa nafasi ya
kuomba uraia lakini walioomba ni wachache na amesema tatizo hilo
linaidhalilisha nchi kutokana na baadhi ya watendaji ikiwemo idara ya
uhamiaji ambao wamekuwa ni sehemu ya tatizo kwa kushindwa kuchukua hatua
kwa wakati.
Rais Kikwete amesema Tanzania siyo shamba la bili ambalo kila mtu
anaweza kuingia na kufanya analotaka na kwamba tatizo hilo la wahamiaji
haramu lisipodhibitiwa sasa litaleta matatizo makubwa ya mipaka na
utawala katika wilaya zote za mkoa wa Kagera kwa miaka ijayo ambapo
watanzania watakosa mahali pa kuishi ndaniya nchi yao kwani wageni
watakuwa wengi zaidi na watakuwa na sauti kuliko wenyeji.
Chanzo Cha Habari: ITV TANZANIA

No comments:
KARIBU UTOE MAONI YAKO HAPA